SERIKALI YAINGILIA KATI MGOGORO WA STAND UNITED



Na Arone Mpanduka, Dar es salaam
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeamua kuingilia kati mgogoro wa kimaslahi unaoiandama klabu ya Stand United ya Shinyanga na kutaka kamati iliyoundwa na mkuu wa mkoa wa Shinyanga kukaa pembeni ili klabu hiyo isimamie yenyewe fedha za udhamini.

Mgogoro huo wa kimaslahi uliibuka baada ya kampuni ya Acacia kujitokeza na kuidhamini timu hiyo na kisha mkuu wa mkoa wa Shinyanga Ali Lufunga  kuunda kamati maalum ya kusimamia fedha za udhamini kwa kuamini kwamba zitatumika vizuri bila kuchakachuliwa.

Hata hivyo maamuzi hayo yaliibua mgogoro mkubwa ambapo viongozi na wadau wa Stand walikuja juu na kushinikiza fedha hizo ziwe zinapitia mikononi mwa klabu.

Akizungumza mapema leo hii Waziri wa Habari, Utamaduni, Wasanii na Michezo Nape Nnauye alisema amezungumza na viongozi wa klabu hiyo kuhusiana na sakata hilo na anaamini kwamba kukaa pembeni kwa kamati hiyo kutaondoa mgogoro huo.


“Huenda Mkuu wa Mkoa alikuwa na nia njema lakini sasa kwa hali jinsi ilivyo sasa inabidi yeye na Kamati yake wakae pembeni na suala hili libaki mikononi mwa klabu,”alisema Nape.

"Ninadhani tatizo kubwa lilikuwa ni hilo, kwa hiyo tusubiri matokeo ya uamuzi huu na kisha tuone  nini kitatokea"

Kwa upande wa uongozi wa Stand United umeelezea kuridhishwa na uamuzi huo. 

Mwenyekiti wa klabu hiyo Amani Vicent alisema kwa hatua hiyo anaamini mgogoro uliopo utamalizika na timu itarejea katika kiwango chake cha awali.

“Kuna wakati kiwango cha timu kilianza kushuka kwa sababu ya hii migogoro lakini sasa naona itarejea kwenye uwezo wake wa awali,”alisema Amani.

Share on Google Plus

About MPANDUKA BLOG

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment

0 comments:

Post a Comment