Mamlaka ya Mapato Tanzania TRA imekamata magari
matano ya Shirikisho la soka nchini TFF kutokana na malimbikizo ya kodi
yanayofikia kiasi cha shilingi bilioni 1.118.
Akizungumza na MPANDUKA BLOG mchana wa leo(Alhamis Machi 31) Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa mlipa kodi wa TRA,
Richard Kayombo amethibitisha kwamba kodi wanayowadai TFF ni mchanganyiko
ambayo haikulipwa kuanzia kipindi cha mwaka 2010 hadi 2015.
Amesema hapo nyuma walikamata akaunti zao kwasababu deni
lilikuwa ni bilioni 1.6 na wakaweza kupunguza sehemu ya deni lakini bado
halijaisha na ndiyo sababu ya kukamata hayo magari matano.
Kwa mujibu wa Kayombo, magari hayo yapo kwenye yadi
ya YONO likiwemo basi ambalo hutumiwa kuisafirisha timu ya taifa ‘Taifa Stars’.
Hii ni mara ya pili kwa TFF kupigiwa hodi na TRA
ikilalamikiwa kulimbikiza madeni ya kodi, mara ya kwanza TRA ilizifunga account
zote za TFF lakini safari hii wameamua kuyashikilia magari yao.
![]() |
| Hili ni basi la Taifa Stars ambalo nalo limekamatwa na TRA |
Mwaka huu unaonekana kuanza vibaya kwa TFF ambapo
hivi sasa kocha mkuu wa Taifa Stars Charles Mkwasa analidai Shirikisho hilo
zaidi ya shilingi milioni 200 ikiwa ni fedha za malimbikizo ya mishahara ya
miezi nane na posho za kujikimu.
Mbali na hilo kuna taarifa zinadai kwamba wachezaji
wa timu ya soka ya taifa ya wanawake Twiga Stars hawakukamilishiwa malipo ya
posho zao hasa baada ya kucheza mchezo wa pili wa marudiano dhidi ya Zimbabwe.
NB; Kwa taarifa zaidi sikiliza kipindi cha michezo cha KUTOKA VIWANJANI cha Redio Tumaini leo kuanzia saa 1;00 usiku. Ni 96.5 FM ama www.tumainimedia.com


0 comments:
Post a Comment